kambi ya upasuaji

MOI yaendesha kambi maalum ya upasuaji wa vibiongo

Na Mwandishi wetu- MOI
Taasisi ya Tiba ya Mifupa Muhimbili (MOI) imeendesha kambi maalum ya upasuaji mkubwa kwa mbinu za kisasa ya mgongo uliopinda (Kibiongo) kwa kushirikiana na madaktari bingwa kutoka marekani ambapo zaidi ya watoto 6 watafanyiwa upasuaji mkubwa.

Mkurugenzi mtendaji wa MOI Dkt Respicious Boniface amesema hii ni sehemu ya mkakati wa Serikali ya awamu ya Sita inayoongozwa na Mh Dkt. Samia Suluhu Hassan wa kuhakikisha huduma zote za kibingwa zinapatikana hapa nchini.

“Tuko hapa kwenye vyumba vya upasuaji MOI ambapo tumepokea jopo la madaktari bingwa na wabobezi kutoka Marekani na Italia ambao watatoa mafunzo kwa wataalamu wetu hapa MOI pamoja na kufanya upasuaji “ alisema Dkt Boniface.

Naye Mkufunzi kutoka Marekani Prof Alaa Azmil Ahmed amesema ni heshima kubwa kupata nafasi na kubadilishana ujuzi na wataalam wa MOI kwani pamoja na kuleta ujuzi mpya kuna mbinu ambazo wanajifunza kutoka kwa madaktari bingwa wa MOI.

Kwa upande wake Daktari bingwa wa Mifupa wa watoto Dkt. Bryson Mcharo ameishukuru serikali ya awamu ya sita pamoja na uongozi wa MOI kwa kuhakikisha mafunzo haya ya yanafanyika mara kwa mara jambo ambalo limepelekea wagonjwa kupata huduma bora hapa nchini bila kulazimika kwenda nje ya nchi.

Taasisi ya MOI imekua ikitekeleza kwa vitendo agizo la Serikali ya awamu ya Sita la kuhakikisha huduma zote za kibingwa za mifupa, ubongo, mgongo na mishipa ya fahamu zinapatikana hapa nchini.

About the Author

You may also like these