KISUTU GIRLS BLOOD DRIVE

Historia yaandikwa katika kampeni ya Kisutu Girls Blood Drive

Na Mwandishi wetu- MOI
Zaidi ya Wanafunzi 1000 kutoka Shule mbalimbali za Sekondari jijini Dar es Salaam leo wamejitokeza katika tukio la uchangiaji damu wa hiari liliofanyika katika viwanja vya shule ya Kisutu ambapo zaidi ya chupa 600 za damu zimepatikana.

Tukio hilo la uchangiaji damu wa hiari limeratibiwa na shule ya Sekondari ya Wasichana Kisutu kwa kushirikiana na Taasisi ya tiba ya Mifupa Muhimbili –MOI na kushirikisha Taasisi ya Damu Salama, Hospitali ya Taifa Muhimbili pamoja na mhamasishaji wa uchangiaji damu Bi. Halima Kopwe ambaye ni Mrembo wa Tanzania kwa mwaka 2022/2023

Mgeni rasmi wa tukio hilo alikua Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Dkt. Rashid Mfaume ambaye alimuwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam ambapo ametoa rai kwa Taasisi zingine kuiga mfano wa Shule ya Wasichana Kisutu na Taasisi ya MOI kwani uhitaji wa damu ni mkubwa katika hospitali mbalimbali nchini.

“Kwa mwaka hapa nchini zinahitajika zaidi ya Chupa zaidi ya elfu ishirini na sita (26,000) ili kuwasaidia majeruhi mbalimbali wa ajali za barabarani, Wagonjwa wa Saratani, Watoto wenye Vichwa vikubwa na mgongo wazi wazazi wanaojiofungua na wahanga wengine hospitalini, hivyo naishukuru sana Taasisi ya MOI na Shule ya Sekondari ya Kisutu kwa kubuni kampeni hii” amesema Dkt. Mfaume

Kwa upande wake Meneja Uhusiano MOI Bw. Patrick Mvungi amesema Taasisi ya MOI itaendelea kubuni matukio mbalimbali ya uchangiaji damu kwa kushirikiana na wadau mbalimbali nchini ili kuhakikisha hakuna mgonjwa anayekosa pindi inapohitajika.

Naye, Mkuu wa Shule ya Wasichana Kisutu Bi. Chiku Mhando amesema lengo la kampeni hii ni kuunga mkono juhudi za Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuondoa changamoto ya tiba damu katika hospitali zilizopo nchini.

“Leo Tumekusanya zaidi ya Wanafunzi 1000 kutoka shule mbalimbali katika mkoa wa Dar es Salaam ambao wamechangia damu kwa hiari kwa lengo la kuwasaidia wagonjwa wenye uhitaji wa damu hospitalini, kwa namna ya pekee naomba nitoe shukrani kwa Taasisi ya MOI, Halotel, CRDB na wadau wengine waliosaidia kufanikisha tukio hili” amesema Bi. Chiku

Tukio la Kisutu Girls Damu drive limekua la kipekee kwani limeweza kuunganisha zaidi ya wanafunzi 1000 kutoka shule za Sekondari zaidi ya 40 katika jiji la Dar es Salaam.

About the Author

You may also like these